Saturday, April 1, 2017

Muendelezo wa njia za kuondoa sumu mwilin


9. Pata usingizi wa kutosha kila siku

Moja ya vitu vinaweza kukupelekea kuwa na sumu mwilini au takataka nyingi ni  pamoja na kutokulala muda wa kutosha kila siku. Usingizi haukopwi na huwezi kuwa na ufanisi katika kazi zako kama hupati usingizi wa kutosha kila siku.

Usingizi siyo jambo la starehe tu, ni sehemu mhimu sana katika afya yako ya kila siku.

Bila kupata usingizi wa kutosha unaweza kuwa karibu na matatizo kama kuongezeka uzito, kushuka kwa kinga ya mwili na nguvu zako za mwili kwa ujumla zinaweza kushuka.

Unapopata muda wa kutosha wa kulala masaa 7 mpaka 8 kwa siku unaupa mwili wako nafasi ya kutosha ya kupumzika na kujiripea upya na hivyo ndivyo sumu na takataka nyingine zinavyoweza kukutoka kirahisi.  Ingia kulala mapema walau saa tatu usiku ingia kulala siyo unakaa unaangalia tamthiliya au mpira mpaka saa sita za usiku!

10. Epuka mazingira hatarishi kwa sumu

Kuna mazingira yanajulikana wazi kuwa ni vyanzo vya sumu mwilini. Maeneo ya migodi ya madini, maeneo yenye viwanda vingi, maduka yanayouza dawa za kilimo nk

Maeneo haya yanafaa kukaa mbali na makazi ya binadamu kwa usalama wa afya zetu.

11. Tumia mtindi

Moja ya njia nyingine ya kuondoa sumu na takataka nyingine ni kutumia vyakula vyenye bakteria wazuri (probiotics). Mtindi ndicho chakula pekee kinajulikana kuwa na bakteria hawa wazuri kwa ajili ya tumbo lako. Pata mtindi kikombe kimoja kila siku na utabaki na mwili msafi muda wote.

Tumia mtindi wa nyumbani ndiyo mzuri zaidi ingawa hata wa dukani nakuruhusu utumie hasa ule ambao haujaongezwa kingine chochote ndani yake (flavors and additives).

12. Epuka vyakula vilivyokobolewa

Ili kuwa na mwili msafi kabisa epuka kula mkate mweupe, sukari na vyakula vinavyopikwa katikati ya mafuta mengi kama vile chipsi, maandazi na vingine vyote vinavyochomwa katikati ya mafuta mengi.

Mkate upo mkate mweusi (brown bread), sukari ipo asali mbichi, vyakula vinavyopikwa katikati ya mafuta mengi unaweza kuamua kuwa unavioka (bake) au uvichemshe (boiling). Uchaguzi ni wako.

13. Ondoa mfadhaiko (stress)

Kile tayari unajuwa ni kuwa mfadhaiko au stress ni jambo baya kwa afya yako. Kile unatakiwa kujua kuanzia sasa ni kuwa ili kubaki na afya bora kabisa yenye TBS basi ukae mbali na stress. Kama utaruhusu stress kutawala maisha yako basi ujuwe mwili wako hauwezi kufanya kazi zake vizuri ikiwemo ya kuondoa taka au sumu mbalimbali mwilini.

Stress peke yake inaweza kupelekea magonjwa mbalimbali mwilini zaidi ya 50. Unapokuwa na mfadhaiko mwili wako hauwezi kutoa taka nje kirahisi na kinga yako ya mwili inashuka matokeo yake unakuwa karibu na magonjwa mengine mengi.

Watu wengine wenye uelewa mdogo wakiwa na stress hukimbilia kutumia vilevi wakidhani zitapungua kumbe ndiyo wanazidi kuongeza tatizo bila kujua. Vitu viwili vinaondoa stress bila kulazimika kutumia njia mbaya kwa afya yako ni mazoezi ya viungo na tendo la ndoa. Siku nyingine ukijiona umefadhaishwa sana nenda kafanye mazoezi ya kufa mtu ikiwezekana baadaye tafuta mtu shiriki tendo la ndoa.

14. Tumia dawa za asili badala ya zile za kizungu

Dawa nyingi za hospitali huwa zina matokeo chanya (positive) na matokeo hasi (negative) pia ambayo ndiyo matokeo mabaya. Kama unalazimika kutumia antibiotic kila mara au unameza dawa za kuondoa maumivu kila mara unaweza kuwa unaongeza sumu na taka mwilini bila kujua na bila sababu yoyote ya lazima.

Kuepuka hilo jaribu kutumia mitishamba au mimea ya asili kwa baadhi ya magonjwa ambayo si lazima uende hospitali. Siyo mafua tu mtu ameenda kuchoma sindano!

15. Acha vilevi

Moja ya vitu vinavyoweza kuleta sumu au taka mwilini moja kwa moja ni vilevi. Vilevi kama pombe, madawa ya kulevya, sigara, bangi na vinginevyo ni vitu vinavyopelekea mwili kuwa na taka moja kwa moja.

Namna pekee ya kuondoa sumu kutokana na vilevi ni kuviacha hivyo vilevi, ndiyo kuviacha. Usitegemee asubuhi utumie dawa kuondoa sumu mwilini halafu jioni ukanywe pombe au ukavute sigara utegemee tu ile dawa uliyotumia asubuhi kwamba itafanya kazi, hapana unajidanganya, dawa ni kuacha vilevi moja kwa moja.

Vingine vya kuacha kama tayari imegundulika una sumu nyingi mwilini ni pamoja na vinywaji baridi vyote, juisi zote za dukani, chai ya rangi na kahawa.

16. Tumia vifuatavyo kuondoa sumu zaidi

Vifuatavyo vinaondoa sumu kirahisi zaidi mwilini; kitunguu swaumu, unga wa majani ya mlonge na mbegu zake na mbegu za maboga au unga wake.
Kitunguu swaumu
Mlonge
Mbegu za maboga

No comments:

Post a Comment